Wednesday, August 5, 2015

JUKWAA LA KATIBA TANZANIA (JUKATA) LAMTAKA RAISI KIKWETE ATOE TAMKO

Jukwaa la Katiba Tanzania (Jukata), wamemtaka Rais Jakaya Kikwete atoe tamko na
kulitangazia Taifa juu ya kukwama kwa mchakato wa Katiba mpya kabla ya kuondoka madarakani, kwa kuwa ukimya uliopo hivi sasa kuhusu mchakato huo ni giza nene kwa Taifa.

Aidha, Jukata limesema kwa kuwa Rais Kikwete ndiye aliyeuanzisha mchakato huo, anapaswa pia kuandaa makubaliano kwa serikali ya awamu ya tano itakayoingia madarakani ili isitekeleze Katiba mpya.
Kadhalika, Jukata limetoa wito kwa viongozi wa vyama vya siasa nchini, kukutana kabla ya kuingia katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu na kukubalina kuhusu kuendelezwa kwa mchakato huo, ili chama chochote kitakachoshinda kifuate utaratibu na makubaliano hayo.

Kaimu Mwenyekiti Jukata, Hebron Mwakagenda (pichani), alisema kuwa ukimya usio rasmi wa mamlaka zinazohusika ikiwamo Wizara ya Katiba na Sheria, kuwapo kwa sheria zilizopitwa na wakati, kuvunjwa kwa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kutoendelea kwa mazungumzo baina ya vyama vya siasa pamoja na kuvunjwa kwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba kumesababisha ombwe la uratibu na mchakato mzima wa katiba hiyo.

“Mchakato huu kwa kuwa ulianzishwa na Rais ni vyema akalitangazia Taifa kusitishwa kwake. Kuna ukimya uliopo kwa Wizara ya Katiba na Sheria, hivyo mchakato huu uliotumia mabilioni ya fedha, umewafanya Watanzania wasifahamu nini kinachoendelea na asasi pekee iliyobaki katika kulizungumzia hili ni sisi Jukata,” alisema Mwakagenda.

Alisema kuvunjwa kwa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambalo linajukumu la kutunga sheria hizo kumefanya mchakato mzima ukwame.

“Siku 60 za utoaji elimu, siku 30 za kampeni, muda wa usajili wa kamati za kura ya maoni, muda wa kutoa taarifa kwa umma juu ya utaratibu wa kuendesha kura ya maoni vimeshindwa kutekelezeka, hivyo awamu ya tano ya serikali isije ikatupeleka katika kura ya maoni kwanza tuitishe mkutano wa kitaifa,’’ alisema Mwakagenda.

Alisema mjadala huo wa kitaifa kabla ya kupigwa kwa kura ya maoni, ushirikishwaji wa asasi za kiraia pamoja na kupatikana kwa muafaka kati ya vyama vya siasa na kurejea mazungumzo yaliyoanzishwa na Rais Kikwete.

No comments :

Post a Comment