Wednesday, August 12, 2015

TBS: TAARIFA KWA UMMA NA WAAGIZAJI WA MAGARI TOKA NJE YA NCHI

Shirika la viwango Tanzania (TBS) lilianzisha huduma ya kukagua magari yaliyotumika kutoka nje ya nchi tangu mwaka wa 2002. Lengo ni kuhakikisha magari yaliyotumika yanayoagizwa kutoka nje ya nchi yanakidhi kiwango cha magari yaliyotumika na yanafaa kuendeshwa barabarani. TBS imekuwa ikipata mawakala wa ukaguzi wa magari nje ya nchi kwa kutangaza zabuni za kimataifa.

Kupima ubora wa bidhaa yakiwemo magari kwenye nchi zinakotengenezwa au kutoka kabla ya kusafirishwa kuingia nchini husaidia kujua bidhaa hizo yakiwemo magari kama yamekidhi kiwango, na kuwa hazina hatari kwa afya ya watumiaji na mazingira. Huduma hii hurahishisha uingizwaji wa bidhaa na kuvikinga viwanda vya ndani dhidi ya ushindani usio halali kutokana na uingizwaji wa bidhaa hafifu.

Shirika la Viwango Tanzania (TBS) linapenda kuufahamisha umma wa Watanzania na waagizaji wa magari yaliyotumika kutoka nje ya nchi kuwa TBS wamesaini hati ya makubaliano na Taasisi ya Usafirishaji ya Taifa (NIT), kwa ajili ya upimaji wa magari yote ambayo hayakukaguliwa ubora wake katika nchi yalipotoka kabla ya kuingia nchini Tanzania. Hivyo kuanzia tarehe 01-07-2015, NIT wataanza rasmi kupima magari yote yaliyoingia nchini bila kukaguliwa.

No comments :

Post a Comment