Friday, June 26, 2015

Maalim Seif azuiwa kuhudhuria Shein akivunja Baraza la Wawakilishi leo

Zanzibar. Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi, wamemzuia Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad kuhudhuria shughuli ya kuvunja Baraza hilo itakayoongozwa na Rais Dk Ali Mohamed Shein leo.

Uamuzi huo ulitolewa baada ya Spika wa Baraza hilo, Pandu Ameir Kificho kutoa utangulizi kwa wajumbe akiwataka watengue kanuni ili viongozi wa kitaifa watakaohudhuria shughuli hiyo waweze kuingia ukumbini badala ya kukaa sehemu ya kawaida ya wageni waalikwa.

Baada ya kutoa utangulizi, Spika Kificho alianza kuwahoji wajumbe wanaokubali viongozi wa kitaifa waruhusiwe kuingia ndani ya Ukumbi wa Baraza kwa kuwataja wakiwamo Rais wa Zanzibar, Jaji Mkuu wa Zanzibar, Omar Othman Makungu, mpambe wa Rais na kuungwa mkono kwa kupigiwa makofi na sauti za ndiyo.

Hata hivyo, alipomtaja Makamu wa Kwanza wa Rais, Maalim Seif Sharif Hamad wajumbe wote waliokuwapo katika Baraza hilo, ambao wote ni wa CCM, walikataa wakisema kwa sauti “hapana,” kitendo ambacho kilimfanya Spika kurudia kutamka jina hilo kwa zaidi ya mara tatu na majibu yalikuwa hapana.

Hatua ya wawakilishi kumkataa Maalim Seif, imekuja siku moja baada ya mawaziri na wajumbe wa CUF kutoka nje ya Baraza wakisusa kujadili na kupitisha muswada wa sheria wa bajeti kuu ya matumizi ya Serikali ya mwaka wa fedha 2015/16 wakipinga pamoja na mambo mengine, mchakato unaoendelea sasa wa uandikishaji wapigakura katika Daftari la Kudumu.

“Mnakubali kutengua kanuni kuruhusu viongozi wa kitaifa kuhudhuria katika shughuli yetu ndani ya ukumbi? Wageni wetu ni Rais wa Zanzibar, mpambe wake, Jaji Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais,” alihoji Spika Kificho lakini alipingwa baada ya kulitaja jina la Makamu wa Kwanza wa Rais.

Awali, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Mohamed Aboud Mohamed aliwasilisha hati ya Serikali kuhusu marekebisho ya kanuni za Baraza.

Waziri Aboud alisema, Rais wa Zanzibar atakagua gwaride maalumu la Polisi kabla ya kuhutubia Baraza hilo saa 9.30 alasiri na kuwataka wajumbe wote kufika kabla ya kuwasili kwa Rais.

Kuhusu uamuzi wa kumkataa Maalim Seif, Aboud alisema upo katika mamlaka ya wajumbe kwa mujibu wa kanuni za Baraza hilo na kwamba hatua itakayofuata ni Spika kumwandikia barua Maalim Seif ya kutohudhuria shughuli hiyo ili kulinda uamuzi wa baraza hilo.

“Baraza ni chombo cha kikatiba, Serikali hatuna uwezo wa kuliingilia na kanuni ndivyo zinavyosema. Wageni ambao ni viongozi wa kitaifa lazima utengue kanuni kwa kuwauliza wajumbe kama wanakubali au kukataa,” alisema.

Waziri Aboud alisema SMZ haitaongeza muda wa Baraza ili kutoa nafasi ya Mwakilishi wa Kwa Mtipura (CCM), Hamza Hassan Juma kuwasilisha hoja binafsi ya kutaka wananchi waulizwe kama wanataka kuendelea na mfumo wa sasa wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK) au la akisema kwa mujibu wa ratiba ya kikao cha bajeti, muda umemalizika na kumtaka kuangalia hoja yake katika siku za baadaye.
 source: Mwananchi

No comments :

Post a Comment