Tuesday, August 18, 2015

TFDA YAPIGA MARUFUKU VIPODOZI 31 VINAVYOZALISHWA NCHINI





Mamlaka ya Chakula na Dawa Tanzania (TFDA), imevifutia usajili vipodozi 31 jamii ya losheni na krimu vinavyotengenezwa na viwanda vya nchini.

Hatua hiyo imefuatia kubainika kuwa na viambato vilivyopigwa marufuku, ambavyo vina athari kubwa kwa watumiaji.

Baadhi ya vipodozi hivyo ni Lovely Body Cream, Baby Soft Body Lotion, Podoa Body Cream, BOSS Hand & Body Cream, CITIZEN Moisturizing Cream, Vestiline Body Lotion, Cocoa Butter Cream, Baby & Me Body Cream na Skala Papaya Body Cream.

Viwanda vinavyotengeneza vipodozi hivyo ni kiwanda cha Chemi & Cotex Industries Limited na Tridea Cosmetics Limited vilivyopo Dar es Salaam, Tanga Pharmaceutical & Palstics Limited (Tanga) na Johnsons & Johnson (Pvt) Ltd cha Afrika Kusini.

Mkurugenzi Mkuu TFDA, Hiiti Sillo, aliyasema hayo jana jijini Dar es Salaam wakati akizungumza na waandishi wa habari.

Alisema pamoja na kuvifutia usajili vipodozi hivyo, pia viwanda hivyo vimetakiwa kutovitengeneza vipodozi hivyo kwa miezi sita, kuviondoa sokoni na kuviteketeza kwa gharama zao.

Sillo alisema viambato vya aina ya ‘steroids’ ambavyo vimo katika vipodozi hivyo vinatumika kama dawa ya kutibu magonjwa mbalimbali ya ngozi, dawa ambazo hazitakiwi kutumika zaidi ya wiki mbili.

“Dawa hizi hutumika kutibu magonjwa ya ngozi na hazitakiwi kutumika bila ya kupewa ushauri na daktari, kwani dawa hizi zikitumika bila ushauri zina madhara kama ngozi kubabuka, kusinyaa, shinikizo la damu kwenye macho, vidole kufa ganzi na kusikia kuzunguzungu na kichefuchefu,” alisema Sillo.

Vipodozi vingine vilivyopigwa marufuku ni White Musk Hydrating Lotion, Aloe vera Softy Body Cream, Johnson’s baby lightly Fragranced Aqueous Cream, Star Rose Lotion, na Skala For Men Body Lotion.

Vingine ni Ella Moisturising Carrot hand & Body Cream, Beauty Care Carrot Cream, Freshia Body Lotion, Star Rose Advanced Moisturising Cream, Goldy Beauty Cream na Skala Carrot Body Cream.

Pia alitoa wito kwa wananchi kutotumia vipodozi hivyo kuanzia leo na kuwa TFDA inaendelea na ukaguzi ili kubaini kuwapo kwa vipodozi vya aina hiyo sokoni pamoja na kuwachukulia hatua za kisheria watakaojihusisha na utengenezaji, usambaji na uuzaji wa vipodozi hivyo.

No comments :

Post a Comment