Thursday, July 9, 2015

Kingunge amtolea uvivu Nape Nnauye

Dodoma. Mwanasiasa mkongwe wa CCM, Kingunge Ngombale-Mwiru amemshukia Katibu wa Itikadi na Uenezi wa chama hicho, Nape Nnauye kwa kauli zake alizodai zinaminya demokrasia na kwamba CCM haiwezi kusimama wanapopambana wenyewe kwa wenyewe.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa jana, Kingunge (pichani), ambaye hivi karibuni aliweka bayana kumuunga mkono Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa katika harakati zake za kuwania urais, alisema hakubaliani na kauli ya Nape kuwa wagombea wasioridhika na uamuzi wa Kamati Kuu (CC), hawawezi kukata rufaa kwa sababu ya muda kuwa mfupi.
Alisema CCM imeweka utaratibu wa wanachama kudai haki zao ndani ya chama, pindi wasiporidhishwa na uamuzi wa vikao vya chini.
Alisema mwaka 2005, mgombea wa nafasi ya urais, John Malecela alikata rufaa katika Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) baada ya jina lake kutopelekwa.
“Aliyekuwa mwenyekiti wa chama wakati ule Mkapa (Benjamin), alikubali baada ya kushauriana na wenzake kwa sababu haikuwa zawadi, bali ni haki yake,” alisema.
Hata hivyo, alisema baada ya kujielezea mbele ya NEC na wajumbe kuulizwa, walikubali kuwa majina matano yaliyoletwa na CC yanatosha.
“Kufikiria kwamba mtu akose haki kwa sababu ya kukosa muda huko ni kuwakosesha watu haki,” alisema.
Kingunge alisema amani na utulivu ni mambo yanayojengwa kwa haki na lazima imani ijengwe na viongozi.
Alisema lugha za kibabe ambazo zimekuwa zikitolewa na baadhi ya viongozi huku chama kikaa kimya ndizo zinazowatia watu shaka.
“Sasa hivi kumekuwa na nguvu kubwa ya kupambana ndani ya chama kuliko wapinzani… nyumba ikigawanyika haiwezi kusimama na CCM haiwezi kusimama inapopambana yenyewe kwa yenyewe,” alisema.
Alisema kukiwa kuna jitihada za kunyima haki watu, kunaweza kusababisha machafuko.
“Asitokee mtu akadhani kuwa nchi ni yake pekee yake, sitaki kusema kwa sababu matokeo yake mnayajua. CCM ni yetu sote hata sisi tuliokuwapo tangu zamani,” alisema. “Ukisema wagombea hawataweza kukata rufaa unapotosha misingi, kwa nini unataka kuminya haki hiyo sasa? Ingekuwa wakati wetu na Mwalimu (Julius Nyerere), mtu wa namna hiyo tungemvua uongozi.”
Hata hivyo, Nape alipoulizwa alisema hawezi kujibu tuhuma hizo kwa kuwa hajamsikia na anayetakiwa kuzijibu ni aliyempa kazi.
“Siwezi kujibu kwa sababu sijamsikia, sijui kasema wapi, amesema nini na kama amesema mimi siwezi kujibu mwenye wajibu huo ni aliyenipa kazi,” alisema Nape.

No comments :

Post a Comment