Thursday, July 9, 2015

KUFUATIA AJALI YA CHOPA: Nassari asimulia ajali

Arusha. Wakati Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari akisema anashindwa kuamini kilichotokea na kunusurika katika ajali ya helikopta juzi, mmiliki wa chopa hiyo, Philemon Ndesamburo amesema atanunua nyingine haraka kabla ya kuanza kampeni za Uchaguzi Mkuu.
Kauli hizo zilitolewa jana ikiwa ni siku moja baada ya helikopta hiyo
inayomilikiwa na Ndesamburo kupitia kampuni yake ya Keys Aviation kupata ajali wakati ikitumiwa na Nassari na baadhi ya viongozi wa Chadema.
Wakati ikipata ajali, ilikuwa imekodishwa na Kampuni ya General Aviation Services (T) Ltd inayomilikiwa na Kapteni William Slaa.
Katibu wa Ndesamburo, Basil Lema alisema ilipata ajali baada ya kupigwa na kimbunga wakati anga likiwa limefunikiwa na wingu zito.
“Mheshimiwa Ndesamburo amemshukuru Mungu kwa kuwanusuru watu waliokuwa kwenye ndege hiyo ambao ni pamoja na Mbunge Joshua Nassari.
“Ameweka wazi kwamba atalazimika kununua nyingine mapema kwa ajili ya kuongeza nguvu kwenye kampeni za Uchaguzi Mkuu mwaka huu,” alisema Lema akimnukuu Ndesamburo.
Lema alisema rubani aliyekuwa akiendesha helikopta hiyo alifanikiwa kuielekeza juu ya miti alioutumia kupunguza kasi ya kushuka chini na kusaidia abiria kutoka salama.
“Imeharibika lakini abiria wote ni wazima. Walikuwamo wanne,” alisema na kuongeza kuwa helikopta hiyo ndiyo iliyotumiwa na Chadema katika Uchaguzi Mkuu wa 2010 na Uchaguzi wa Serikali za Mitaa mwaka jana na chama hicho kilitegemea kuitumia katika Uchaguzi Mkuu ujao.
Pia, imewahi kutumiwa na makada mbalimbali wa CCM akiwamo Naibu Katibu Mkuu wa CCM, Mwigulu Nchemba na kada maarufu wa Moshi mjini, Buni Ramole.
Kauli ya Nassari
Akizungumza na waandishi wa habari katika wodi alikolazwa kwenye Hospitali ya Seliani – Arusha, Nassari alisema waliporuka kutoka Leguruki, hakukuwa na dalili zozote za kuchafuka kwa hali ya hewa, lakini dakika chache baada ya kuruka angani wingu zito lililoambatana na upepo mkali liliwafunika ghafla.
“Wingu lile na upepo ule sijawahi kuona katika maisha yangu yote zaidi ya kusoma kwenye vitabu vya simulizi vya mambo ya ushirikina. Namshukuru Mungu wote tuko salama kwani hatukuwa na matumaini ya kupona ajali ile,” alisema Nassari.
Mbunge huyo aliyekuwa katika ziara ya kuhamasisha wananchi kujiandikisha kwenye Daftari la Wapigakura, alimwagia sifa rubani Slaa kwa uwezo na ustadi aliouonyesha hadi wakanusurika.
“Kama siyo ustadi wake, naamini watu wangeokota vipande vya nyama tu kwenye eneo la ajali, ila Mungu ni mkuu leo tuko hai wote licha ya madhara madogo,” alisema.
Nassari alisema muda mfupi kabla ya kuruka saa kumi na moja jioni, wakati akihutubia mkutano huko Leguruki, alipokea simu kutoka kwa mchungaji mmoja akimtaarifu kupata maono kuwa anakabiliwa na hatari ya kukutwa na jambo kubwa na baya akimtaka adumu katika sala.
“Dakika 15 baadaye nikaruka na kupata ajali. Naamini kilichotuokoa ni nguvu ya sala niliyosali baada ya kupokea ujumbe wa mchungaji na maombi ya wachungaji wangu wanaoniombea kila siku,” alidai Nassari.
Rubani Slaa alisema alishangaa lilipotokea wingu na upepo uliosababisha ndege kuanguka ikiwa njiani kuelekea Ndoombo na Ngureserosambu.
“Kabla ya kurusha ndege nilijiridhisha na hali ya hewa. Hakukuwa na kiashiria chochote cha hali ya hatari kama maeneo mengine ambako tulishindwa kutua kutokana na mvua zilizokuwa zikinyesha.
Kaimu Mkurugenzi wa Hospitali ya Seliani, Dk Paul Kisanga alisema hali za majeruhi si mbaya, isipokuwa Eva Kayaha aliyevunjika mbavu mbili.

No comments :

Post a Comment