Friday, July 31, 2015

Meya Mwanza matatani kwa rushwa

Meya wa Jiji la Mwanza, Stanslaus Mabula
Chanzo: Imeandikwa na Moses Mseti-Mwanza , Mwanahalisi Online
Meya anaemaliza muda wake, jijini Mwanza, Stanslaus Mabula, anatuhumiwa kuwahonga
vijana fedha, kuwafanyia fujo na kuwatembezea kichapo wagombea wenzake. Meya huyo anatuhumiwa na wagombea wenzake wanane kati ya 18 (majina yanahifadhiwa) kwamba amekuwa akifanya mchezo mchafu wa kuwahonga vijana kuwafanyia fujo ikiwemo fujo iliyofanyika juzi Jumatano.
Inaelezwa Meya Mabula ambaye ni Diwani wa Kata ya Mkolani, anawafanyia mchezo huo wagombea wenzake ili wasipate nafasi ya kujinadi na kujieleza kwa Wana CCM .
“Juzi (Jumatano) wiki hii tulikuwa kwenye kata mpya ya Luchelele ambayo anataka kugombea safari hii, tukiendelea na mikutano ya hadhara na wagombea wenzagu lakini ghafra ilitokea gari aina ya Noah iliyokuwa imebeba vijana na kuanza kutukimbiza.
“Vijana hawa walitukimbiza wakati tunaelekea kupanda gari tulilokuwa tumekwenda nalo. Tulikimbia mpaka tukaacha gari letu kwa sababu ya mtu mmoja kweli,” amesema mgombea huyo ambaye hakutaka kutajwa jina lake.
Hata hivyo Amesema Mabula anatumia mbinu hizo chafu kwa sababu anafahamu kuwa hawezi kuingia katika hatua ya tatu bora na kwamba ndo maana anawahonga vijana kuwafanyia fujo.
Mgombea huyo alienda mbali kwamba Mabula anatumia mchezo huo kwani anafahamu safari hii hata nafasi ya udiwani hawezi kuitetea katika uchaguzi wa mwaka huu hivyo analazimika kupambana kwenye ubunge.
Amesema umefika wakati kwa wagombea wa chama hicho kuacha kutumia nguvu ya fedha kuwashawishi watanzania kuwachagua katika nafasi zao ili kuwapata viongozi walio bora.
“Suala hili Mkoa mzima wanalifahamu na hata viongozi wa chama wanalifahamu. Kama tukiendelea na utaratibu wa wagombea ubunge na udiwani kutumia fedha kuingia madarakani kamwe hatutaweza kuwa na viongozi ambao ni bora kwa maendeleo ya Taifa,” amesema.
Hata hivyo mgombea huyo anaetajwa kuwa na ushawishi mkubwa ndani na nje ya chama na anayepewa nafasi kubwa ya kupeperusha bendera ya chama hicho katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu, aliwaomba wagombea wenzake kufanya siasa zisizo na chuki.
Meya wa Jiji hilo anaemaliza muda wake, Stanslaus Mabula ambaye ni mlalamikiwa, alipotafutwa na gazeti hili kupitia simu yake ya mkononi alimtaka Mwandishi kumpigiwe baadae kwa madai yupo kwenye kikao ambacho hakukitaja jina na alipotafutwa simu yake haikupokelewa.
Hata hivyo kwa mjibu wa kanuni na sheria za uchaguzi inaelezwa mgombea wa nafasi yeyote ile ya udiwani ubunge na Urais haruhusiwa kutumia viashiria vyovyote vile vinavyoashiria rushwa lakini hali ipo tofauti kwa meya huyo ambaye anaendesha mashindano ya Meya Cup yanayoendelea jijini hapa.

No comments :

Post a Comment