Monday, August 3, 2015

Mnyika aibukia Kamati Kuu



Naibu Katibu Mkuu wa Chadema Bara, John Mnyika (wa kwanza kushoto) akiwa na viongozi wenzake katika kikao cha Kamati Kuu ya Chadema kilichofanyika leo jijini Dar es Salaam


MBUNGE wa Ubungo, John Mnyika, ameibuka jijini Dar es Salaam na kuhudhuria kikao
cha Kamati Kuu (CC) ya chama chake. Taarifa kutoka ndani ya kikao cha CC kinachofanyika katika hoteli ya Bahari Beach zinasema, Mnyika amehudhuria mkutano huo  siku ya jana tarehe 2/ 08  na kueleza kuwa kutoonekana kwake, kumetokana na matatizo ya familia.

Mnyika ambaye ni naibu katibu mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), amekuwa haonekani tangu Edward Lowassa alipojiunga na chama chake, Jumapili iliyopita.

Mbali na Mnyika, katibu mkuu wa chama hicho, Dk. Willibrod Slaa, hajaonekana katika ofisi za chama hicho, tangu Lowassa ajiunge na Chadema; jambo ambalo limezua taharuki kwamba huenda amejiuzulu wazifa wake.

Dk. Slaa ambaye alishiriki vikao vyote muhimu na majadiliano vilivyomkaribisha Lowassa ndani ya Chadema, anadaiwa kuzuiwa na mkewe, Josephine Mushumbuzi, kushughulika na chama hicho.

Mwanasheria mkuu wa Chadema, Tundu Lissu amethibitisha Mnyika kuhudhuria mkutano huo.

Amesema, “…Mnyika yupo ndani ya ukumbi wa mkutano. Anashiriki kikao cha kamati kuu. Waliokuwa wanadhani chama chetu kimepata mpasuko kutokana na ujio wa Lowassa, walikuwa wanajidanganya.”

Lissu amesema, ndani ya Chadema wako wamoja, yote yaliyotokea yalikuwa mapambano yanayotokana na ukomavu wa kidemokrasia uliyopo.


No comments :

Post a Comment