Saturday, June 27, 2015

Dk Shein, Maalim Seif wapishana kauli waliosusia Baraza la Wawakilishi

Tokeo la picha la dr. sheinZanzibar/Dar. Wakati Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Seif Sharif Hamad, ameunga mkono kitendo cha mawaziri na wajumbe wa CUF kususia baraza, Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein amekipinga.

Kauli tofauti za viongozi hao wa ngazi ya juu katika Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK), zimekuja baada ya mawaziri na wawakilishi wa CUF kutoka ndani ya Baraza la Wawakilishi, wakisusia kujadili muswada wa Sheria wa Bajeti Kuu ya matumizi ya Serikali ya mwaka wa fedha 2015/2016.

Akizungumza na Mwananchi jana, Maalim Seif alisema wajumbe waliona njia sahihi ya kufanya ni kutoka ndani ya baraza, kwa sababu walikuwa hawasikilizwi kila wanapozungumzia mchakato unaoendelea kwa sasa wa uboreshaji wa daftari la kudumu la wapigakura.

Maalim alisema anashangazwa na wajumbe wa baraza kushindwa kujadili hoja iliyojitokeza, kiasi cha kusababisha baadhi ya wajumbe kususia kikao cha bajeti.

Alisema alisema kwamba tangu kuanza kwa uandikishaji, kumekuwa na mambo yanayofanyika kinyume kabisa na sheria, yakiwamo watoto chini ya umri wa miaka 18 kuandikishwa katika daftari la wapiga kura, vyombo vya ulinzi na usalama kutumika kutisha watu huku wakiwa wamevaa ‘kininja’, jambo ambalo ni kinyume na utaratibu.

“Ni wazi inaonyesha kwamba kuna kasoro kwenye uandikishaji wananchi kwenye daftari la kudumu na usajili wa Vitambulisho vya Mzanzibar mkazi,” alisema.

Kuhusu Serikali ya Umoja wa Kitaifa, SUK, Maalim Seif alisema kwamba haiwezi kuvunjika, kwa sababu hakuna wa kuivunja kwa kuwa ilipitishwa kwenye Azimio la Baraza la Wawakilishi.

Hivyo, ikiwa inatakiwa kuvunjwa ni lazima, Serikali ifuate sheria ya kuanza mchakato wa Kura za Maoni, kuuliza wananchi watoe maoni yao na kisha kufikisha tena kwenye Baraza la Wawakilishi waijadili.

Pia alisema wanasiasa wanaojadili suala la kuendelea au kutokuendelea kwa SUK, wanastahili kujiuzulu au kufukuzwa ndani ya vyama vyao.

Alisema kuwa, hoja ya CCM kutaka kufuta SUK inapaswa kulaaniwa kwani italeta machafuko Zanzibar.

“Serikali ya Umoja wa Kitaifa si ya CCM wala CUF tu, ni ya wananchi wote, ni makosa makubwa kudhani kuwa Serikali hiyo ni ya vyama hivyo viwili. Ilifanyika hivyo ili kutokuendelea umwagaji damu,” alisema.

“Tangu asubuhi kwa hapa Zanzibar ilifahamika kabisa kwamba nitazuiwa kuingia kwenye kikao cha Baraza la Wawakilishi hata watoto walijua ‘’alisema.
Source: Mwananchi

No comments :

Post a Comment